Enekia, Nyota wa Twiga Stars ajiunga na timu ya Ligi Kuu Mexico

tiga stars

Baada ya kutamba kwenye ligi kuu za nchi mbalimbali kuanzia Tanzania, Morocco na Saudi Arabia, nyota wa kimataifa wa Tanzania, Enekia Lunyamila amejiunga na klabu ya Mazaltan inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake nchini Mexico kwa mkataba wa miaka miwili.

Kiraka huyo msimu uliopita alikuwa akiitumikia Eastern Flames ya Saudia ambayo ilimaliza nafasi ya saba kati ya timu nane zinazoshiriki Ligi ya Wanawake nchini humo.

Msimu uliopita Mazaltan ambayo ni timu mpya ya Enekia ilimaliza nafasi ya 14 kati ya 18 zilizoshiriki Ligi hiyo baada ya kucheza mechi 17, ikishinda minne, sare moja na kupoteza 12.

Mchezaji huyo baada ya kujiunga na klabu hiyo ataungana na Mtanzania mwenzake, beki wa kati Julietha Singano anayekipiga Juarez ya nchini humo.

Kwa mujibu wa takwimu zilizoripotiwa na gazeti la Mwanaspoti hadi sasa Lunyamila amefunga mabao 110 kwenye ligi mbalimbali, akiwa na Alliance Girls mwaka 2016 alifunga mabao 37, Ruvuma Queens (2018) mabao 27 huku Ausfaz Assa Zag ya Morocco akifunga mabao 49 mwaka 2021 akiibuka na tuzo ya mfungaji bora na mabao saba akiifungia Eastern Flames ya Saudia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *