Roberto Gabriel Trigo: Mchezaji aliyeangusha ndege kwa shuti la mpira

Roberto Gabriel Trigo, ni mchezaji wa soka wa zamani kutokea nchini Paraguay ambaye mwezi Februari mwaka 1957 alifanya jambo la kustaajabisha.

Mzee huyu pengine ndiye mtu pekee aliye hai anayeweza kuthibitishia ulimwengu kwamba shuti lake la mpira alilopiga miaka ya nyuma liliwahi kuangusha ndege ndogo iliyokuwa ikipita angani.

Roberto alikuwa na umri wa miaka 17 wakati huo akicheza kama beki wa kulia kwenye klabu ya ‘General Genes’ kwenye jiji la Asuncion.

Akiwa amekerwa na ndege hiyo ndogo iliyokuwa ikipita mara kwa mara maeneo ya uwanja waliokuwa wakifanyia mazoezi, Trigo alikamata mpira na kupiga shuti lililopiga maeneo ya engine ya ndege hiyo na kusababisha kuanguka katika eneo la wazi, umbali wa kama mita 200 tu toka mahali alipokuwa amesimama.

Mtu aliyekuwa akiendesha ndege hiyo ni Alfredo Lird, shabiki mkubwa timu ya ‘General Genes’ na mtu ambaye Trigo alikuwa akimfahamu vyema.

Alfredo alikuwa na tabia ya kuruka chini sana kwenye uwanja wa mpira wakati wa mazoezi na michezo rasmi, na kila mara walimtania kwamba kuna siku wangeiangusha ndege yake na hakuna mtu aliyefikiria kwamba Trigo angeweza kufanya hivyo.

“Kwa muda kidogo mchezo ulisimama. Niliingiwa na hofu…..walinichukua na kuninywesha maji ya baridi na mengine kunimwagia kichwani..wakiniambia: ‘usijali, hakuna kilichotokea hata kidogo, rubani yuko sawa’. Kwa hiyo nilianza kutulia,” Trigo anakumbuka.

Lird alikuwa yeye na mtoto wake wa kiume mdogo ndani ya ndege hiyo lakini wote walitoka salama bila majeraha yoyote.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *