TIMU YA DARAJA LA PILI MISRI KUKIPIGA NA SIMBA LEO

KOCHA Mkuu wa Simba,Fadlu Davids leo anatarajia kujaribu siraha zake dhidi ya El Qanah inayoshiriki ligi daraja la pili nchini Misri.

Simba itakuwa ni mechi yao ya kwanza ya kirafiki kucheza tangu walipotua nchini Misri katika jiji la Ismailia walipoweka kambi wiki mbili zilizopita kwa ajili ya maandalizi ya msimu wa 2024/25.

Kocha Fadlu amesema baada ya mazoezi ya wiki mbili na kucheza mechi ya ndani ya wenyewe kwa wenyewe sasa anahitajj kuona kile anachowapa wachezaji kimefuata kwa kiasi gani.

Amesema kuna vitu ambavyo anahitaji kuona kwa wachezaji wake ikiwemo mbinu na ufundi katika nafasi zote ikiwemo umakini wa mabeki na washambuliaji lakini akihitaji mchezo wa spidi.

“Baada ya mazoezi ya wiki mbili na kucheza mechi za wenyewe kwa wenyewe, leo tutacheza mechi ya kirafiki na timu pinzani (El Qanah FC), baada ya hapo tutakuwa na mechi mbili zingine jumla tutakuwa na mechi tatu,” amesema kocha huyo.

Amesema mechi hizo tatu zitamsaidia kuona ubora na madhaifu ya kikosi chake kusahihisha makosa ambayo atakayaona katika michezo hiyo mitatu kabla ya mechi ya Simba Day.

“Baada ya hizo mechi tutarejea nyumbani kujiandaa na sherehe zetu za Simba Day na kufanya vizuri katika mchezo huo naamini mashabiki wanahitaji kuona timu yao ikifanya vizuri,”amesema kocha huyo.

Kuelekea sherehe za Simba zinazotarajiwa kufanyika Agosti 3, mwaka huu uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam, wanatarajia kucheza na APR FC.

Imeelezwa kuwa APR ya Rwanda itacheza mchezo huo wa kurafiki ambao utakuwa maalum wa kutambulisha wachezaji wapya , jezi na benchi la ufundi linaloongozwa na Kocha Fadlu.

Meneja wa idara ya habari ya wasiliano wa Simba, Ahmed Ally amesema wataweza wazi ni timu gani watacheza nao katika mechi yao ya kirafiki ya kimataifa siku ya sherehe yao.

“Ile Ubaya Ubwela itazinduliwa Agosti 3, mwaka huu tutaweka wazi tutacheza na timu gani, baada ya hapo ubaya Ubwela itaenda kufanya kazi Agosti 8, katika mchezo wetu dhidi ya Yanga,” amesema Ahmed.

Kuhusu sakata la Mshambuliaji wao, Denis Kibu, ameweka wazi kuwa kinachokwamisha nyota huyo kuchelewa kuingia kambini ni changamoto cha hati ya kusafiria ambayo imejaa.

“Hayo maneno ya kuwa Kibu anatudai ndio maana hajaenda nchini Misri ni uongo, nyota huyo hatudai hata pumzi kwa sababu tumemlipa kile alichokihitaji katika mkataba wake. Akimaliza changamoti hizo atajiunga kambini,” amesema Ahmed.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *